Biblia Habari Njema

Yohane 12:27-43 Biblia Habari Njema (BHN)

27. “Sasa roho yangu imefadhaika, na niseme nini? Je, niseme: ‘Baba, usiruhusu saa hii inifikie?’ Lakini ndiyo maana nimekuja – ili nipite katika saa hii.

28. Baba, ulitukuze jina lako.” Hapo sauti ikasema kutoka mbinguni, “Nimelitukuza, na nitalitukuza tena.”

29. Umati wa watu waliokuwa wamesimama hapo walisikia sauti hiyo, na baadhi yao walisema, “Ni ngurumo.” Lakini wengine wakasema, “Malaika ameongea naye!”

30. Lakini Yesu akawaambia, “Sauti hiyo haikutokea kwa ajili yangu mimi, ila kwa ajili yenu.

31. Sasa ndio wakati wa ulimwengu huu kuhukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atapinduliwa.

32. Nami nitakapoinuliwa juu ya nchi nitamvuta kila mmoja kwangu.”

33. (Kwa kusema hivyo alionesha atakufa kifo gani).

34. Basi, umati huo ukamjibu, “Sisi tunaambiwa na sheria yetu kwamba Kristo atadumu milele. Wawezaje basi, kusema ati Mwana wa Mtu anapaswa kuinuliwa? Huyo Mwana wa Mtu ni nani?”

35. Yesu akawaambia, “Mwanga bado uko nanyi kwa muda mfupi. Tembeeni mngali mnao huo mwanga ili giza lisiwapate; maana atembeaye gizani hajui aendako.

36. Basi, wakati mnao huo mwanga uaminini ili mpate kuwa watu wa mwanga.” Baada ya kusema maneno hayo, Yesu alikwenda zake na kujificha mbali nao.

37. Ingawa Yesu alifanya miujiza hii yote mbele yao, wao hawakumwamini.

38. Hivyo maneno aliyosema nabii Isaya yakatimia:“Bwana, nani aliyeuamini ujumbe wetu?Na uwezo wa Bwana umedhihirishwa kwa nani?”

39. Hivyo hawakuweza kuamini, kwani Isaya alisema tena:

40. “Mungu ameyapofusha macho yao,amezipumbaza akili zao;wasione kwa macho yao,wasielewe kwa akili zao;wala wasinigeukie, asema Bwana,ili nipate kuwaponya.”

41. Isaya alisema maneno haya kwa sababu aliuona utukufu wa Yesu, akasema habari zake.

42. Hata hivyo, wengi wa viongozi wa Wayahudi walimwamini Yesu. Lakini kwa sababu ya Mafarisayo, hawakumkiri hadharani kwa kuogopa kwamba watatengwa na sunagogi.

43. Walipendelea kusifiwa na watu kuliko kusifiwa na Mungu.