Biblia Habari Njema

Luka 18:1-19 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Basi, Yesu aliwasimulia mfano kuonesha kwamba ni lazima kusali daima bila kukata tamaa.

2. Alisema: “Katika mji mmoja kulikuwa na hakimu ambaye hakuwa anamcha Mungu wala kumjali binadamu.

3. Katika mji huohuo, kulikuwa pia na mama mmoja mjane ambaye alimwendea huyo hakimu mara nyingi akimwomba amtetee apate haki yake kutoka kwa adui yake.

4. Kwa muda mrefu huyo hakimu hakupenda kumtetea huyo mjane; lakini, mwishowe akajisemea: ‘Ingawa mimi simchi Mungu wala simjali binadamu,

5. lakini kwa vile huyu mjane ananisumbua, nitamtetea; la sivyo ataendelea kufika hapa, na mwisho atanichosha kabisa!’”

6. Basi, Bwana akaendelea kusema, “Sikieni jinsi alivyosema huyo hakimu mbaya.

7. Je, ndio kusema Mungu hatawatetea wale aliowachagua, ambao wanamlilia mchana na usiku? Je, atakawia kuwasikiliza?

8. Nawaambieni atawatetea upesi. Hata hivyo, je, kutakuwako na imani duniani wakati Mwana wa Mtu atakapokuja?”

9. Halafu Yesu aliwaambia pia mfano wale ambao walijiona kuwa wema na kuwadharau wengine.

10. “Watu wawili walipanda kwenda hekaluni kusali: Mmoja Mfarisayo, na mwingine mtozaushuru.

11. Huyo Mfarisayo akasimama, akasali kimoyomoyo: ‘Ee Mungu, nakushukuru kwa vile mimi si kama watu wengine: Walafi, wadanganyifu au wazinzi. Nakushukuru kwamba mimi si kama huyu mtozaushuru.

12. Nafunga mara mbili kwa juma, natoa zaka sehemu ya kumi ya pato langu.’

13. Lakini yule mtozaushuru, akiwa amesimama kwa mbali bila hata kuinua macho yake mbinguni, ila tu akijipiga kifua kwa huzuni, alisema: ‘Ee Mungu, unionee huruma mimi mwenye dhambi.’

14. Nawaambieni, huyu mtozaushuru alirudi nyumbani akiwa amesamehewa. Lakini yule mwingine, sivyo. Kwa maana kila anayejikweza atashushwa, na kila anayejishusha atakwezwa.”

15. Watu walimletea Yesu watoto wadogo ili awawekee mikono yake. Wanafunzi walipowaona, wakawazuia kwa maneno makali.

16. Lakini Yesu akawaita kwake akisema: “Waacheni hao watoto waje kwangu, wala msiwazuie, kwa maana ufalme wa Mungu ni kwa ajili ya watu kama hawa.

17. Nawaambieni kweli, mtu yeyote asiyeupokea ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo, hataingia katika ufalme huo.”

18. Kiongozi mmoja, Myahudi, alimwuliza Yesu, “Mwalimu mwema, nifanye nini ili niweze kuupata uhai wa milele?”

19. Yesu akamwambia, “Mbona waniita mwema? Hakuna aliye mwema ila Mungu peke yake.