Biblia Habari Njema

Yohane 3:21-33 Biblia Habari Njema (BHN)

21. Lakini mwenye kuuzingatia ukweli huja kwenye mwanga, ili matendo yake yaonekane yametendwa kwa kumtii Mungu.”

22. Baada ya hayo, Yesu alifika mkoani Yudea pamoja na wanafunzi wake. Alikaa huko pamoja nao kwa muda, akibatiza watu.

23. Yohane pia alikuwa akibatiza watu huko Ainoni, karibu na Salemu, maana huko kulikuwa na maji mengi. Watu walimwendea, naye akawabatiza.

24. (Wakati huo Yohane alikuwa bado hajafungwa gerezani.)

25. Ubishi ulitokea kati ya baadhi ya wanafunzi wa Yohane na Myahudi mmoja kuhusu desturi za kutawadha.

26. Basi, wanafunzi hao wakamwendea Yohane na kumwambia, “Mwalimu, yule mtu aliyekuwa pamoja nawe ngambo ya Yordani na ambaye wewe ulimshuhudia, sasa naye anabatiza, na watu wote wanamwendea.”

27. Yohane akawaambia, “Mtu hawezi kuwa na kitu asipopewa na Mungu.

28. Nanyi wenyewe mwaweza kushuhudia kuwa nilisema: ‘Mimi siye Kristo, lakini nimetumwa ili nimtangulie!’

29. Bibi arusi ni wake bwana arusi, lakini rafiki yake bwana arusi, anayesimama na kusikiliza, hufurahi sana anapomsikia bwana arusi akisema. Ndivyo furaha yangu ilivyokamilishwa.

30. Ni lazima yeye azidi kuwa maarufu, na mimi nipungue.”

31. Anayekuja kutoka juu ni mkuu kuliko wote; atokaye duniani ni wa dunia, na huongea mambo ya kidunia. Lakini anayekuja kutoka mbinguni ni mkuu kuliko wote.

32. Yeye husema yale aliyoyaona na kuyasikia, lakini hakuna mtu anayekubali ujumbe wake.

33. Lakini mtu yeyote anayekubali ujumbe wake anathibitisha kwamba Mungu ni kweli.