Biblia Habari Njema

Yohane 12:12-23 Biblia Habari Njema (BHN)

12. Kesho yake, kundi kubwa la watu waliokuja kwenye sikukuu walisikia kuwa Yesu alikuwa njiani kuja Yerusalemu.

13. Basi, wakachukua matawi ya mitende, wakatoka kwenda kumlaki; wakapaza sauti wakisema:“Sifa! Abarikiwe huyo ajaye kwa jina la Bwana.Abarikiwe mfalme wa Israeli.”

14. Yesu akampata mwanapunda mmoja, akapanda juu yake kama yasemavyo Maandiko:

15. “Usiogope mji wa Siyoni!Tazama, Mfalme wako anakuja,amepanda mwanapunda!”

16. Wakati huo wanafunzi wake hawakuelewa mambo hayo, lakini Yesu alipokwisha tukuzwa, ndipo walipokumbuka kwamba hayo yalikuwa yameandikwa juu yake, na kwamba watu walikuwa wamemtendea hivyo.

17. Kundi la watu wale waliokuwa pamoja na Yesu wakati alipomwita Lazaro kutoka kaburini, akamfufua kutoka kwa wafu, walimshuhudia.

18. Kwa hiyo umati huo wa watu ulimlaki, maana wote walisikia kwamba Yesu alikuwa amefanya ishara hiyo.

19. Basi, Mafarisayo wakaambiana, “Mnaona? Hatuwezi kufanya chochote! Tazameni, ulimwengu wote unamfuata.”

20. Kulikuwa na Wagiriki kadhaa miongoni mwa watu waliokuwa wamefika Yerusalemu kuabudu wakati wa sikukuu hiyo.

21. Hao walimwendea Filipo, mwenyeji wa Bethsaida katika Galilaya, wakasema, “Mheshimiwa, tunataka kumwona Yesu.”

22. Filipo akaenda, akamwambia Andrea, nao wawili wakaenda kumwambia Yesu.

23. Yesu akawaambia, “Saa ya kutukuzwa kwa Mwana wa Mtu imefika!