Biblia Habari Njema

Yohane 11:18-36 Biblia Habari Njema (BHN)

18. Kijiji cha Bethania kilikuwa karibu na Yerusalemu, umbali upatao kilomita tatu.

19. Wayahudi wengi walikuwa wamefika kwa Martha na Maria kuwafariji kwa kifo cha kaka yao.

20. Basi, Martha aliposikia kwamba Yesu alikuwa anakuja, akaenda kumlaki; lakini Maria alibaki nyumbani.

21. Martha akamwambia Yesu, “Bwana, kama ungalikuwa hapa, kaka yangu hangalikufa!

22. Lakini najua kwamba hata sasa chochote utakachomwomba Mungu, atakupa.”

23. Yesu akamwambia, “Kaka yako atafufuka.”

24. Martha akamjibu, “Najua kwamba atafufuka wakati wa ufufuo, siku ya mwisho.”

25. Yesu akamwambia, “Mimi ndimi ufufuo na uhai. Anayeniamini mimi hata kama anakufa, ataishi;

26. na kila anayeishi na kuniamini, hatakufa kamwe. Je, waamini hayo?”

27. Martha akamwambia, “Ndiyo Bwana! Mimi naamini kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni.”

28. Baada ya kusema hayo, Martha alikwenda kumwita Maria, dada yake, akamwambia faraghani, “Mwalimu yuko hapa, anakuita.”

29. Naye aliposikia hivyo, akainuka mara, akamwendea Yesu.

30. Yesu alikuwa hajaingia kijijini, ila alikuwa bado mahali palepale Martha alipomlaki.

31. Basi, Wayahudi waliokuwa nyumbani pamoja na Maria wakimfariji walipomwona ameinuka na kutoka nje ghafla, walimfuata. Walidhani alikuwa anakwenda kaburini kuomboleza.

32. Basi, Maria alipofika mahali pale Yesu alipokuwa na kumwona, alipiga magoti, akamwambia, “Bwana, kama ungalikuwa hapa, kaka yangu hangalikufa!”

33. Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliokuja pamoja naye wanalia pia, alijawa na huzuni na kufadhaika moyoni.

34. Kisha akawauliza, “Mlimweka wapi?” Wakamwambia, “Bwana, njoo uone.”

35. Yesu akalia machozi.

36. Basi, Wayahudi wakasema, “Tazameni jinsi alivyompenda!”