Biblia Habari Njema

Yohane 1:1-14 Biblia Habari Njema (BHN)

1. Hapo mwanzo, Neno alikuwako; naye alikuwa na Mungu, naye alikuwa Mungu.

2. Tangu mwanzo Neno alikuwa na Mungu.

3. Kwa njia yake vitu vyote viliumbwa; hakuna hata kiumbe kimoja kilichoumbwa pasipo yeye.

4. Yeye alikuwa chanzo cha uhai na uhai huo ulikuwa mwanga wa watu.

5. Na mwanga huo huangaza gizani, nalo giza halikuweza kuushinda.

6. Mungu alimtuma mtu mmoja jina lake Yohane,

7. ambaye alikuja kuwaambia watu juu ya huo mwanga. Alikuja ili kwa ujumbe wake watu wote wapate kuamini.

8. Yeye hakuwa huo mwanga, ila alikuja tu kuwaambia watu juu ya huo mwanga.

9. Huu ndio mwanga halisi, mwanga unaokuja ulimwenguni, na kuwaangazia watu wote.

10. Basi, Neno alikuwako ulimwenguni, na kwa njia yake ulimwengu uliumbwa, lakini ulimwengu haukumtambua.

11. Alikuja katika nchi yake mwenyewe, nao walio wake hawakumpokea.

12. Lakini wale waliompokea, wale waliomwamini, aliwapa uwezo wa kuwa watoto wa Mungu,

13. ambao walizaliwa si kwa maumbile ya kibinadamu, wala kwa nguvu za kimwili, wala mapenzi ya mtu, bali kutokana na Mungu mwenyewe.

14. Naye Neno akawa mwanadamu, akakaa kwetu. Nasi tumeuona utukufu wake, utukufu wake yeye aliye Mwana wa pekee wa Baba; amejaa neema na ukweli.