Biblia Habari Njema

Luka 13:18-32 Biblia Habari Njema (BHN)

18. Yesu akauliza: “Ufalme wa Mungu unafanana na nini? Nitaulinganisha na nini?

19. Ni kama mbegu ya haradali aliyotwaa mtu mmoja na kuipanda shambani mwake; ikaota na kuwa mti. Ndege wa angani wakajenga viota vyao katika matawi yake.”

20. Tena akauliza: “Nitaulinganisha ufalme wa Mungu na nini?

21. Ni kama chachu aliyoitwaa mama mmoja na kuichanganya pamoja na unga madebe mawili na nusu kisha unga wote ukaumuka.”

22. Yesu aliendelea na safari yake kwenda Yerusalemu huku akipitia mijini na vijijini, akihubiri.

23. Mtu mmoja akamwuliza, “Je, Mwalimu, watu watakaookoka ni wachache?”

24. Yesu akawaambia, “Jitahidini kuingia kwa kupitia mlango mwembamba; maana nawaambieni, wengi watajaribu kuingia lakini hawataweza.

25. Wakati utakuja ambapo mwenye nyumba atainuka na kufunga mlango. Nyinyi mtasimama nje na kuanza kubisha mlango mkisema: ‘Bwana, tufungulie mlango.’ Lakini yeye atawajibu: ‘Sijui mmetoka wapi.’

26. Nanyi mtaanza kumwambia: ‘Sisi ndio wale tuliokula na kunywa pamoja nawe; na wewe ulifundisha katika vijiji vyetu.’

27. Lakini yeye atasema: ‘Sijui nyinyi mmetoka wapi; ondokeni mbele yangu, enyi nyote watenda maovu.’

28. Ndipo kutakuwa na kulia na kusaga meno, wakati mtakapowaona Abrahamu, Isaka na Yakobo na manabii wote wapo katika ufalme wa Mungu, lakini nyinyi wenyewe mmetupwa nje!

29. Watu watakuja kutoka mashariki na magharibi, kutoka kaskazini na kusini na kukaa kwenye karamu katika ufalme wa Mungu.

30. Naam, wale walio wa mwisho watakuwa wa kwanza; na wale walio wa kwanza watakuwa wa mwisho.”

31. Wakati huohuo, Mafarisayo na watu wengine walimwendea Yesu wakamwambia, “Ondoka hapa uende mahali pengine, kwa maana Herode anataka kukuua.”

32. Yesu akawajibu, “Nendeni mkamwambie huyo mbweha hivi: ‘Leo na kesho ninafukuza pepo na kuponya wagonjwa, na siku ya tatu nitakamilisha kazi yangu.’