Biblia Habari Njema

2 Wafalme 8:14-20 Biblia Habari Njema (BHN)

14. Ndipo Hazaeli alipotoka kwa Elisha, akarudi kwa bwana wake. Mfalme Ben-hadadi akamwuliza, “Elisha alikuambia nini?” Hazaeli akamjibu, “Aliniambia ya kwamba hakika utapona.”

15. Lakini kesho yake Hazaeli akachukua blanketi akalilowesha majini, kisha akamfunika nalo usoni mpaka akafa. Hazaeli akatawala Aramu mahali pake.

16. Mnamo mwaka wa tano wa utawala wa Yoramu mwana wa Ahabu, mfalme wa Israeli, Yehoramu mwana wa Yehoshafati, mfalme wa Yuda alianza kutawala.

17. Alianza kutawala akiwa na umri wa miaka thelathini na miwili. Alitawala huko Yerusalemu miaka minane.

18. Alizifuata njia mbaya za wafalme wengine wa Israeli, kama jamaa ya Ahabu ilivyofanya, kwa sababu mkewe alikuwa binti Ahabu. Akatenda maovu mbele ya Mwenyezi-Mungu,

19. lakini Mwenyezi-Mungu hakutaka kuangamiza Yuda, kwa sababu ya Daudi mtumishi wake, kwani aliahidi kwamba wazawa wake wataendelea kutawala milele.

20. Wakati wa enzi ya Yehoramu, watu wa Edomu waliasi utawala wa Yuda, wakamtawaza mfalme wao.